Thursday, June 27, 2013

NAMPENDA BIBI


Ni mara kadhaa nimewahi kusikia maneno yakitoka kwenye vinywa vya watu wakisema vibaya juu ya malezi ya akina bibi. Wengi wamekuwa wakiwakataza hata watoto wao kwenda kwa bibi zao kwa madai kuwa, akina bibi wanalea kijukuu hivyo wanawaharibu watoto kwa watawadekeza.

Bibi kwangu naweza kusema ni zaidi ya MLEZI. Nayasema hayo kwa kuwa mimi mwenyewe ni shahidi wa hilo kwa kuwa nimeishi na bibi toka nikiwa na umri wa chini ya miaka mitano hadi kufikia umri wa ujana nilionao.

Kikubwa kwake nilichojifunza ni UPENDO! Siku zote bibi hataki kuona au kusikia mjukuu wake akipata shida siyo kwa sababu anamdekeza mjukuu hapana, ila kwa sababu anampenda mtoto wake hivyo hapendi kuona mwanaye akipatwa na matatizo katika malezi. (wote tunajua ugumu wa malezi kwa watoto ulivyokuwa mgumu).
Na kwa sababu ya upendo huo ndiyo maana anaonekana kwamba hajui kulea, lakini tujue kwamba tunakosea tunapoyasema hayo. Kama wewe umelelewa na huyo huyo mama je inakuwaje akawa mlezi mbaya kwa mwanao!
Na siku zote tunatakiwa kujua kwamba akina bibi hushiriki maumivu ya mtoto wake endapo mtoto wa mtoto wake atapatwa na matatizo.

Bibi mara nyingi alitumia hadithi katika kufundisha mema na mabaya, kweli ni vigumu au ni mara chache sana kumuona bibi akishika fimbo kumchapa mjukuu. Kama akigundua wewe ni mvivu, mbeya, mchoyo, mwizi, una wivu bibi atatumia hekima zake ili kufikisha ujumbe kwako juu ya madhara ya mambo hayo. Mengi niliyokuwa nikiambiwa na bibi nimeyaona kama siyo kwangu mwenyewe kunitokea basi kupitia kwa wenzangu.

Bibi ni mlezi mzuri sana tena sana, kamwe hawezi kushindwa kumlea mwanao. Kama atashishindwa basi hata kwako atakuwa alishindwa.
Hivi karibuni nitawashirikisha wale ambao walikosa nafasi hiyo ya kukaa na bibi kwa mawazo ya wazazi wao kwamba bibi zao wangewaharibu, yale ambayo mimi nimeyapata kwa bibi. kupitia hadithi!!!


NAKUPENDA SANA BIBI, HESHIMA KWA AKINA BIBI WOTE DUNIANI!!!

1 comment: